To Advertise on this Blog please Call: +255 (0)656 56 13 14 or Email: maishablog@yahoo.com                                                 To Advertise on this Blog please Call: +255 (0)656 56 13 14 or Email: maishablog@yahoo.com

Tuesday 22 March 2011

Idadi ya waliokufa kwenye ajari ya five stars modern taarabu yafikia 13!!

NYOTA ya kikundi cha muziki wa taarab cha Five Stars iliyong’ara katika ulimwengu wa muziki imezimika ghafla usiku wa kuamkia leo baada ya gari walilokuwa wakisafiria kupata ajali eneo la Doma mkoani Morogoro na kuua wanamuziki 13 papo hapo.

Ajali hiyo ilitokea saa mbili usiku wakati hicho kikiwa safarini kuja Dar es Salaam kikitokea Mbeya na Iringa kilikofanya tamasha la muziki.

Ajali hiyo ilitokea baada ya gari walimokuwa wakisafiria kuligonga kwa nyuma lori lenye shehena ya mbao lililokuwa limesimama maeneo ya kijiji cha Doma, mpakani mwa mbuga ya wanyama ya Mikumi, Kilosa mkoani Morogoro.

Baadhi ya waliokufa katika ajali hiyo wametajwa kuwa ni pamoja na kiongozi wa bendi hiyo, Nasoro Madenge, Issa Kijoti, Husna Mapande na Sheba Juma (ambaye alikuwa mpiga kinanda)

Wengine ni Hamisa Musa, Omari Hashimu, Omary Hashimu (mpiga gitaa), Tizzo Mgunda, Ramadhan Kinyoa, Omary Tall 'Fundi Mitambo', Haji ‘Mbeba Vyombo’ na
Nassor Madenge (Mhasibu).

Wengine watatu ambao majina yao hayajafahamika, wawili kati yao ni marafiki wa Hummer Q aliyeimba wimbo wa ‘Pembe la Ng'ombe’ ambaye amenusurika katika ajali hiyo baada ya kushuka njiani.

Wengine walionusurika katika ajali hiyo ni Ally Juma 'Ally J', Mwanahawa Ally, Samila, Issa Kamongo, Mwanahawa, Zenna Mohamed, Shaaban Mfupi ' Fundi Mitambo', Rajabu Kondo na mwingine aliyefahamika kwa jina moja la Haji.

Mwenyekiti wa kikundi hicho, Khamis Slim, amesema wamepokea kwa masikitiko taarifa za ajali hiyo hizo na yeye pia amenusurika kwa kuwa hakuwapo kwenye ziara hiyo kwa sababu alikuwa amefiwa.

“Sina cha kuzungumza zaidi, lakini pengo tuliloachiwa ni kubwa mno na nadhani hakuna atakayeweza kuliziba,” amesema Slim na kuongeza, “Tumepoteza vijana wengi wenye uwezo wa hali ya juu wa kisanii. Hili ni pigo kwa kundi, vikundi, taifa na familia pia kutokana na michango yao katika fani hiyo.”

Five Stars imetamba kwa nyimbo za Wapambe Msitujadili (Nchumu nchumu tena mwawah!) wa Musa Kijoti, La Uchungu Halisauliki' (Zenna), Riziki Mwanzo wa Chuki, Shukrani kwa Mpenzi na nyinginezo.

Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Adolphina Chialo, ajali hiyo ilitokea saa 2:30 usiku wa kuamkia leo eneo la kijiji cha Doma wakati gari walilokuwa wakisafiria wasanii hao lenye namba T 351 BGE aina ya Toyota Coaster kuligonga kwa nyuma lori lenye nambari T 848 APE lililokuwa na tela lenye namba T 559 BBE likiwa na shehena ya mbao ambalo lilikuwa limesimama kijijini hapo baada ya kuharibika.

Inadaiwa kuwa gari lililowabeba wasanii hao lilikuwa katika mwendo kasi na lilipojaribu kulipita lori hilo kulitokea lori jingine mbele yaka lililokuwa likitokea Morogoro kwenda Iringa lenye nambari T 530 BHY na tela nambari T 182 BKB ambalo nalo lilikuwa katika mwendo kasi hivyo dereva wa gari la wasanii hao akalazimika kurudi kushoto na kuligonga kwa nyuma lori lililoharibika.

Kamanda wa Polisi Kikosi cha Usalama Barabarani mkoa wa Morogoro, Ibrahim Mwamakula, amesema chanzo cha ajali hiyo ni uzembe wa dereva wa gari la wasanii hao.

Kamanda Mwamakula amesema miili ya marehemu hao imeharibika vibaya kwani mbali na kukandamizwa na vyuma vya gari lao, walichomwa na kutobolewa tobolewa miili yao na mbao zilizokuwa katika roli lililogongwa.

Kamanda Mwamakula amesema wasanii hao walikuwa katika ziara ya kikazi katika wilaya ya Kyela mkoani Mbeya na walikuwa wakirejea baada ya kumaliza ziara hiyo.

Amesema vyombo vya muziki vya wasanii hao vilivyokuwa ndani ya gari hilo vimeharibika kabisa.

Kamanda Mwamakula amesema miili ya marehemu hao imehifadhiwa katika chumba cha kuhifadhia maiti katika Hospitali ya Mkoa wa Morogoro wakati , majeruhi tisa wa ajali hiyo wanaendelea na matibabu hospitalini hapo.

Februari mwaka huu kulitokea taarifa za kikundi hicho kudaiwa kupata ajali maeneo ya Chalinze ambapo ilidaiwa robo tatu ya wasanii wake walifariki dunia.

Wasanii hao walidaiwa kuwa walikuwa wakitoka mikoa ya jirani kwenye onesho la muziki, jambo ambalo baadaye lilibainika kuwa ni uvumi.

Hivi karibuni mtabiri maarufu wa nyota Afrika Mashariki na Kati, Sheikh Yahya Hussein, alitabiri kuwa wasanii maarufu, waandishi maarufu na vigogo watakufa mwaka huu.

Pia aliwahi kutabiri kuwa atatokea mganga ambaye atatoa tiba za magonjwa sugu ukiwamo UKIMWI, utabiri ambao unadaiwa kutimia baada ya kujitokeza mchungaji mstaafu wa KKKT, Ambilikile Mwasapile, wa Loliondo mkoani Arusha.

“Mimi simlengi yeyote katika utabiri wangu, lakini nyota inaonesha kuwa bado hali hiyo itaendelea na kuna uwezekano wa waandishi wa habari kufa,” amesema Sheikh Yahya leo asubuhi.

Hata hivyo, akizungumza kwa njia ya simu amesema amepokea kwa masikitiko taarifa hizo kwa kuwa ni pengo ndani ya jamii kutokana na mchango wa wasanii hao.

Mungu izilaze mahali pema peponi roho za wasanii hawa.

source;DAr leo

No comments: